LATEST HEADLINES👉

Your Ad Spot

Nov 25, 2015

MBUNGE AYSHAROSE AUNGA MKONO UAMUZI WA RAIS DK. MAGUFULI KUHUSU MAADHIMISHO YA SIKU YA UHURU MWAKA HUU

MBUNGE wa Viti Maalum Mkoa wa Singida, Aysharose Mattembe, amesema Rais Dk. John Magufuli ni kiongozi mwenye kujali maslahi ya Watanzania hivyo maamuzi ya kuwataka wananchi kusherehekea kumbukumbu ya Uhuru kwa kufanya kazi na usafi, umeonyesha dhamira safi ya kiongozi huyo kwa wananchi.

Amesema, uamuzi huo umejali maslahi ya taifa kwa sababu fedha nyingi zingetumika kwenye masuala yasiyokuwa na ulazima kwa wananchi.


Pia, ametoa rai kwa watumishi na viongozi wenzake wa serikali kufanyakazi kwa kuwatumikia wananchi ili kuendana na kasi ya Rais Dk. Magufuli.


Akizungumza Dar es Salaam jana, Aysharose alisema, kuzuiliwa kwa fedha hizo kutumika kwenye sherehe za Uhuru ni sahihi kwa sababu baadhi ya watu wamekuwa wakijinufaisha.


Hivyo uamuzi ya Rais Dk. Magufuli ya kupangia fedha hizo matumizi  mengine hususan kuboresha huduma za afya ni wakuungwa mkono.


Aysharose alisema, badala ya fedha hizo kutumika kuwahudumia wageni, kupamba maeneo mbalimbali yatakayotumika kwenye sherehe hizo na kununulia mashati sasa zitatumika kwenye sekta ambayo inaumuhimu kwa maisha ya Watanzania.


“hospitali zetu bado hazina madawa ya kutosha, wahudumu wa afya pia wanafanyakazi kwenye mazingira magumu, shule hazina madawati ya kutosha lakini pia maslahi ya walimu sio mazuri hivyo fedha hizo zitasaidia kuboresha huduma hizo” alisisitiza.


Alisema anaunga mkono maamuzi hayo ya Rais kwa sababu fedha hizo zinakwenda kutatua changamoto wanazokabiliana nazo wananchi.


Mbunge huyo wa viti maalum alibainisha kuwa, baadhi ya watumishi wa umma wamekuwa wakitumia sherehe hizo kujinufaisha binafsi kwenye shughuli yenye kufanyika kwa siku moja.


“Hatuwezi kutumia fedha za walipakodi kwa matumizi yasiyokuwa endelevu hivyo kwa msingi huo, maamuzi ya Rais yamejikita kutumia fedha hizo kwa maendeleo endelevu” alibainisha.


Aysharose ambaye anawawakilisha wanawake wa mkoa wa Singida bungeni, alisema serikali ya awamu ya tano ni ya ukombozi kwa sababu Rais Dk. Magufuli ni imara na mwenye kujali maslahi ya wanyonge.


Alisema Rais. Dk. Magufuli ni mwajibikaji na hatowaonea huruma viongozi wabadhirifu na wala rushwa.


“Serikali ya wamu ya tano inaongozwa na kiongozi mwenye kujali maslahi ya wananchi, wenye uchungu kwa kutaka kufikia maendeleo ya kiuchumi na anadhamira safi ya kuwatumikia Watanzania kwa kuwakomboa wanyonge,” alisema.


Alisisitiza kuwa, Rais Dk. Magufuli, hatoweza kufumbia macho vitendo vitakavyorudisha nyuma maendeleo ya nchi hivyo watumishi wa umma wasiowajibika wanapaswa kukaa chonjo.


Juzi Rais Dk. Magufuli, alizuia kufanyika kwa sherehe za Uhuru Desemba 9 mwaka huu na kuamuru siku hiyo itumike kufanya kazi ikiwemo usafi kwenye maneneo mbalimbali nchini ili kukabiliana na ugonjwa wa kipindipindu.


Kwa mujibu wa agizo hilo la rais lililotolewa na Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue, Rais alisema wananchi hawapaswi kusherehekea miaka 54 ya Uhuru wa Tanzania Bara, huku wakiendelea kufariki kwa ugonjwa huo unaosababishwa na uchafu.


Aliamuru fedha zilizokuwa zitumike kugharamia sherehe hiyo zitapangiwa matumizi mengine ya maendeleo hususan kuboresha huduma za afya.


Uamuzi huo wa rais umeendelea kuungwa mkono na wananchi kwa sababu imechukuliwa ili fedha hizo zitumike kwenye masula muhimu zaidi yenye maslahi ya taifa.

No comments:

Post a Comment

ANDIKA MAONI (COMMENTS) HAPO👇

Post Top Ad

Your Ad Spot

Pages